Blogger Widgets

June 10, 2013

Siri ya Kifo cha Mume wa Khadija Kopa Yagundulika

KIFO cha mume wa Malkia wa Mipasho Bongo, Khadija Omar Kopa, Jaffari Ally ambaye ni Diwani wa Kata ya Magomeni Wilaya ya Bagamoyo, Pwani, kimeibua simulizi ya kusikitisha kufuatia kifo hicho kilivyotokea na maombolezo aliyokuwa akiyatoa malkia huyo wakati akiuaga mwili wa marehemu nyumbani kwao, Bagamoyo, Ijumaa iliyopita.
 
Khadija Omar Kopa akilia kwa uchungu baada ya kuona jeneza lenye mwili wa mumewe, Jaffari Ally.
Khadija aliibua simanzi, vilio pamoja na waombolezaji waliokuwa wakimsikiliza wakati akiuswalia na kuuaga mwili wa mumewe kabla ya kupelekwa makaburini.
Wakati kifo kinatokea, Khadija Kopa alikuwa Sumbawanga kwenye ziara ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohemed Bilal kuhusu mazingira.
Katika tukio hilo, Khadija akiwa ameishiwa nguvu alitamka maneno ya kumtakia pepo njema marehemu mumewe wake huku akisema kwa huzuni:

 
Mwili wa Jaffari ukipelekwa makaburini.
“Mume wangu, sintasahau ulivyokuwa ukinisistiza kujiendeleza katika masomo ya kumuabudu Mungu pia nakumbuka ulivyokuwa ukiniambia mara kwa mara kama umenikosea nikusamehe.
“Mume wangu sikumbuki kama ulinikosea na hata kama ulinikosea nimekusamehe nakuomba nawe kama nilikukosea unisamehe, naahidi kukupenda siku zote za maisha yangu.”
Mmoja wa marafiki wa Khadija aliyekuwa naye muda mfupi kabla ya kifo cha mumewe aliyekuwa amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Lugolo, Dar es Salaam,  alisikika akisema:
“Tulikuwa safarini muda mfupi kabla ya kupata taarifa za kifo, kuna mtu alimpigia simu Khadija na kumwambia kuwa hali ya mumewe ni mbaya na amelazimika kuwekewa mashine ya kumsaidia kupumua (oxygen).
“Hali hiyo ilimfanya Khadija achanganyikiwe na kuanza kulia kisha akakata simu na kuendelea kulia.


 
Mazishi ya marehemu Jaffari.
“Mtu moja aliyekuwa jirani na mgonjwa alimchomoa mashine hiyo ili azungumze na mkewe kwenye simu kwa lengo la kumtia nguvu.
“Baada ya mgonjwa kuchomolewa mashine hiyo, Khadija alipigiwa simu, akaongea na mumewe. Hiyo ilikuwa saa saba usiku kuelekea kifo chake kilichotokea saa tisa usiku.
“Mumewe alimwambia mkewe kwamba anaendelea  vizurio, hajawekewa oxygen kama watu wanavyosema na kumtaka mkewe apige kazi huko aliko.
“Hapo kidogo Khadija alijisikia nafuu, akapata usingizi kwa mbali kabla ya taarifa kamili kwamba saa tisa kwamba mumewe ameaga dunia,” kilisema chanzo hicho.

 
Marehemu Jaffari Ally enzi za uhai wake.
Taarifa zaidi za kusikitisha zinasema kuwa, baada ya kupata taarifa za kifo cha mumewe, Khadija alipoteza fahamu hali iliyosababisha ugumu wa mawasiliano kwa vile baadhi ya viongozi wake kwenye Kundi la Taarab la ToT walimtumia pesa kwa njia ya simu lakini ili kusaidia mambo mbalimbali ambapo ilishindikana kutoa kwa sababu mhusika alikuwa hajitambui.
Marehemu Jaffari alizikwa Juni 7, 2013 kwenye Makaburi ya Mwanakerenge, Bagamoyo, Pwani. Mungu ailaze pema peponi roho ya marehemu. Amina.

From:GPL

No comments:

Post a Comment