Msanii wa filamu Tanzania, Agnes Gerald 'Masogange' alikamatwa na dawa za kulevya Afrika Kusini hivi karibuni.
Serikali imeamua kuanza kuchapisha magazetini picha na majina ya wahusika wa biashara ya dawa za kulevya.
Hatua
hiyo iliyotangazwa jana na Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe
inalenga kuisafisha nchi dhidi ya uchafuzi unaotokana na tatizo hilo.
Sambamba
na kutoa msimamo huo, Dk Mwakyembe jana aliwaambia waandishi wa habari
taarifa ya kukamatwa kwa mtuhumiwa wa dawa hizo katika Uwanja wa Ndege
wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Dar es Salaam.
Mtuhumiwa
huyo Edwin Monyo (39) mwenye pasipoti namba AB 202513 anadaiwa kukutwa
na kete za heroin 86 na misokoto ya bangi 34, juzi usiku akisafiri
kwenda Italia kupitia Zurich, Uholanzi.
Waziri
alikuwa akizungumzia ziara ya ghafla aliyofanya JNIA juzi kwa lengo la
kujiridhisha kuhusu vifaa na taratibu zinazotumika kwa ukaguzi wa
abiria, ili nchi isiwe kichochoro cha kupitisha dawa za kulevya.
Kuhusu
kuchapisha majina na picha, alisema Serikali itakuwa ikifanya hivyo, ili
wahusika wafahamike na hatimaye kukomesha biashara hiyo.
Hata hivyo, alisema leo atatoa taarifa juu ya Watanzania wawili waliokamatwa Hong Kong wakiwa na dawa kama hizo.
“Niliahidi
kutoa taarifa juu ya tukio la Mtanzania aliyekamatwa na dawa hizo hivi
karibuni katika uwanja wa ndege wa Oliver Tambo, Afrika Kusini, lakini
tukabaini kuna wawili wengine waliokamatwa Hong Kong … sasa hatutaji
jina bila kuonesha picha,” alisema Dk Mwakyembe.
Kuhusu
tukio la juzi, alisema mtuhumiwa alikamatwa saa 2:15 usiku ambapo
alikuwa akitarajia kusafiri kwa ndege ya Shirika la Ndege la Uswisi na
kwamba tiketi na hati yake ya kusafiria vinashikiliwa.
Alisema
kwa hatua za ziada, Serikali itaanza utaratibu wa kumulika mizigo yote
itakayokuwa inaingia nchini ili kuhakikisha kelele za dawa za kulevya
zinamalizika.
Katika
hatua nyingine, Dk Mwakyembe aliitaka Mamlaka ya Viwanja vya Ndege
Tanzania (TAA) kuwapandisha daraja na kuwaongeza mishahara watumishi
wawili wa kike waliowezesha kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo.
Alisema
katika ziara yake ya ghafla alibaini kuwapo taratibu zote zinazotakiwa
na kusema tatizo ni watendaji wanaopewa dhamana ya kusimamia ambao
hawatekelezi wajibu wao kikamilifu.
Mwezi
jana wanawake wawili raia wa Tanzania walikamatwa katika uwanja wa ndege
wa Oliver Tambo, Johannesburg, Afrika Kusini, wakidaiwa kuingiza
shehena ya dawa za kulevya zenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 6.8
wakitoka nchini.
Kamanda
wa Polisi wa Kitengo cha Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Geofrey
Nzowa, aliwataja watuhumiwa hao ambao inadaiwa walishafikishwa
mahakamani nchini humo kuwa ni Agnes Gerald 'Masogange' na Melisa
Edward.
No comments:
Post a Comment