Blogger Widgets

August 11, 2013

Soma Mkasa Mzima Waliosimulia Mabinti Watatu waliomwagiwa Tindikali Zanzibar Baada ya Kufika Kwao


Wasichana hao wakisindikizwa hospitalini mara baada ya kuwasili nchini Uingereza juzi.
Majeraha ya mmoja wa wasichana walioshambuliwa kwa tindikali yalizidi kuwa katika hali mbaya baada ya msamaria aliyepagawa kummwagia maji machafu, imebainika.

Taarifa za shambulio hilo la kutisha pia zimefichua wasichana hao wawili raia wa Uingereza, ambao wameunguzwa vibaya baada ya kumwagiwa tindikali, waliwaona washambulizi wao wakitabasamu na kuamkiana kwa kugusanisha vichwa muda mfupi kabla ya kuwamwagia tindikali.
Wafanyakazi wa kujitolea Katie Gee na Kirstie Trup, wote wenye umri wa miaka 18, waliwasili nchini kwao juzi na wakahamishiwa Hospitali ya Chelsea and Westminster mjini London kupatiwa matibabu ya majeraha yao ya moto.
Sam Jones, ambaye alikuwapo kwenye kisiwa hicho cha Zanzibar na rafiki yake wa kike, Nadine wakati huo, alieleza jinsi alivyosikia kelele za uchungu kufuatia shambulio hilo na kukuta mmoja wao amejikunyata kwenye jengo la choo akiwa katika maumivu makali.
Alieleza wasichana hao walisema walikuwa wakitembea kwenye mtaa mmoja ndipo pikipiki yenye wanaume wawili ilipowapita kando yao na kusimama.
Alisema: "Wanaume hao walitazamana, wakagonganisha vichwa na kutabasamu - kisha mmoja wao akawamwagia tindikali kutoka kwenye chombo, kama debe la petroli."
Jones alisema yeye, Nadine na kundi la watu wa mahali hapo walimkuta Katie karibu na jengo la choo akipiga kelele za maumivu.
Alisema: "Nguo zake zichanika kabisa ndani ya dakika chache. Kulikuwa uvundo na harufu kali."
Alisema tindikali hiyo ilikuwa na nguvu mno kiasi cha kumuunguza hata yeye mikononi wakati akijaribu kuwasaidia wasichana hao.
Wapenzi hao walisema waliwasaidia wanawake hao waliojeruhiwa kwa kuambatana nao kwenye ndege binafsi kuelekea jijini Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu.
Wakati huohuo, gazeti la The Times limeripoti jinsi majeraha ya mmoja wa wasichana hao yalivyo mabaya zaidi kuliko mwenzake, sababu wasamaria walitumia maji machafu kwenye majeraha yao ya moto.
Kirstie hatahivyo anafahamika kuwa alipelekwa baharini eneo la jirani na lilipotekea shambulio hilo Mji Mkongwe, katika hoteli moja iliyoko ufukweni, ambapo iliripotiwa kumwokoa na majeraha makubwa zaidi kama aliyopata rafiki yake.
Katie juzi aliwashukuru waliompa msaada kwa salamu zao za kuwatakia afya njema huku wawili hao wakiendelea kupata nafuu hospitalini.
Daktari wao, Andy Williams, mtaalamu wa majeraha ya moto na upasuaji alisema: "Tunaweza kuthibitisha kwamba Katie na Kirstie wamehamishiwa chini ya uangalizi wetu kwenye kitengo cha majeraha ya moto cha Hospitali ya Chelsea and Westminster ambako bado wanatathminiwa majeraha yao.
"Wasichana wote wanaendelea vema na familia zao ziko pamoja nao. Watakaa kwenye Hospitali ya Chelsea and Westminster.
"Familia zote zinapenda kumshukuru kila mmoja ambaye amesaidia kurejeshwa nyumbani wasichana hao.
"Familia hizo kwa sasa zingependa kupata muda wa kuwauguza wasichana hao na kwamba vyombo vya habari vinatakiwa kuheshimu hilo katika kipindi hiki kigumu."
Watu watano wanahojiwa na polisi katika kisiwa hicho kilichopo kwenye Bahari ya Hindi baada ya wanawake hao kushambuliwa wakati wakitembea kando ya barabara Jumatano usiku.
Baba wa Kirstie alisema wasichana hao walikuwa wamevalia inavyotakiwa na walishaonywa wasivae chochote kitakachopingana na historia yao ya Kiyahudi, ikiwamo Nyota ya Daudi.
Alieleza: "Tunafahamu ni nchi ya Kiislamu, wao ni wasichana kutoka Magharibi. Kwa bahati mbaya walikwenda matembezini wakati wa mwezi wa Ramadhani.
"Kumekuwa na tahadhari kubwa katika nchi za Afrika kutokana na kuwapo kwa vitisho. Pengine vinahusiana, au la!
Wasichana hao walishapanga kurejea kwa wakati kwenda kupokea matokeo yao ya A-Level wiki ijayo, huku Kirstir akitarajia kusomea Historia katika Chuo Kikuu cha Leeds, iliripotiwa.
Zanzibar ni kisiwa cha funguvisiwa katika Bahari ya Hindi kilichopo takribani maili 22 kutoka Bara.

No comments:

Post a Comment