Blogger Widgets

January 30, 2014

Soman na Utambue Hapa Sifa Kumi za Mwanamke Asiyefaa Kwenye Ndoa

SUALA la kuoa lipo tu licha ya kwamba wapo wanaochelewa kuingia kwenye maisha hayo wakihisi inaweza kusitisha furaha ya maisha yao. Nasema hivyo kwa kuwa najua wapo wanaoamini kuoa ama kuolewa ni kujiingiza kwenye matatizo.
Dhana hiyo haina mashiko kiviile, asikuambie mtu unapoingia kwenye ndoa na mtu anayekupenda na wewe unampenda kwa dhati, karaha hakuna licha ya kwamba kugombana kwa hapa na pale hakuwezi kukosekana. 

Hata hivyo, nikiri tu kwamba, zipo ndoa ambazo ni ndoano. Yaani unakuta mtu kaingia kwenye ndoa na mtu ambaye hakuwa amedhamiria, matokeo yake kadiri siku zinavyokwenda anahisi ameingia chaka na anaishia kuomba ndoa isiwepo. 

Leo nataka kuwazungumzia wanawake ambao ni majanga na ukijichanganya ukaingia nao kwenye maisha ya ndoa, utakiona cha mtemakuni. 

10. Asiyeridhika na penzi unalompa
Wapo wanawake ambao wewe unaweza kujitahidi kumpatia mapenzi kadiri unavyoweza lakini yeye hatosheki. Anakuchukulia wewe ni dhaifu sana na wakati mwingine kuhisi yupo mwingine anayeweza kumpa zaidi ya kile unachompa, huyu ni tatizo.
 

9. Wivu kupindukia
Hatukatai, wivu ni muhimu sana kwenye suala la mapenzi lakini kuna ule wivu uliopindukia kiasi cha kuwa kero. Walio kwenye ndoa wananielewa namaanisha nini.
Kwa kifupi mtu mwenye mapenzi ya dhati na mwenziye lazima awe na wivu lakini ukiwa na ule wa kupinduki ni tatizo linaloweza kuitibua ndoa.
 

8. Anaona unamsaliti kila mara
Huku kunatokana na kutokujiamini tu. Ukioa mwanamke ambaye kila wakati unapokuwa mbali naye anahisi unamsaliti, huyo hakuamini na kamwe hamuwezi kudumu. Mara kadhaa mtakuwa mkigombana akihisi una mwingine kumbe hakuna ukweli katika hilo.
 

7. Anahisi amekosea kuwa na wewe
Wapo wanawake ambao wanapoingia kwenye ndoa baada ya muda wanahisi wamekosea kuolewa na mwanaume huyo. Unakuta mke wa mtu anahisi fulani ambaye zamani alikuwa kwenye uhusiano naye angekuwa sahihi zaidi baada ya kuona upungufu fulani kwa huyo aliyemuoa.
 

6. Yuko kimasilahi zaidi
Kuna wanawake ambao ukiwaoa wanakuwa na furaha na wewe ukiwa unazo tu, ukiishiwa wanaanza kununa na kuleta visirani vya hapa na pale. Hawa ni tatizo, mwanamke wa kweli ni yule anayeridhika kuwa na wewe kwenye shida na raha.
 

5.Yuko tayari kuachana na wewe
Hivi hujawahi kumsikia mke wa mtu akimwambia mumewe; ‘Kama vipi tuachane, kwanza kwetu sijafukuzwa na nilikuwa nakula, nalala, navaa.” Mwanamke anayeweza kumtamkia mume wake maneno haya, huyo si mke na kamwe hawezi kukufanya uwe na furaha.
 

4. Hapendi ndugu zako
Waswahili wanasema ukipenda boga, penda na ua lake. Kama utatokea kuoa mwanamke ambaye anakupenda wewe tu lakini akija ndugu, rafiki au mtu mwingine wa karibu yako anabadilika, huyo ana matatizo kwani atakufanya utengwe na jamii yako.
 

3. Anajali mafanikio binafsi
Siku zote wawili waliotokea kupendana wakioana wanakuwa mwili mmoja hivyo lazima watakuwa wanawaza na kufanya maamuzi pamoja. 

Ogopa sana mwanamke anayependa kutumia kipato chake kufanya mambo binafsi tena kwa siri. Kwa mfano kusaidia kwao, kujenga nyumba kwao, kuanzisha miradi yake bila kukushirikisha. 

2. Eti akizaa utamzeesha
Hili kwa wale wanaopenda kuoa masistaduu. Wapo ambao wakitajiwa suala la kuzaa mara baada ya kuingia kwenye ndoa wanagoma wakidai eti watazeeshwa hivyo waachwe kwanza wale ujana. Wakati huo unaweza kukuta mwanaume anataka mtoto ili apate ile heshima, mke anagoma kwa sababu hiyo isiyo na msingi, hili ni tatizo.
 

1. Anataka awe na sauti
Mwanaume siku zote atabaki kuwa kiongozi wa familia lakini wapo baadhi ya wanawake hawataki kukubaliana katika hilo. Wengi wanalazimisha usawa na wengine wakitaka wao ndiyo wawe na sauti kuliko waume zao. Hili nalo ni janga! Yaani mkeo anataka kila linalofanyika yeye awe mtu wa kutoa maamuzi! Mh!

No comments:

Post a Comment