Kuna
mambo kusimamiwa kwake kidete ni kukaa chini, mengine ni kulala na
mengine ni kusimama wima. Kukiwa na jambo au hali haulidhiki nayo,
machaguo yako mengi kuonyesha hisia na hata msimamo wako. Yote haya
lazima yafanyike maadamu tu ujumbe ufike kwa ufasaha mahala husika
wakati hatua sahihi zikiendelea na utekelezwaji.
Haiwezekani kwenye nchi yenye tatizo la ajira linaloongezeka kila uchao
vijana wenye vipaji wafe na njaa kisa tu ugomvi na madalali wa sanaa!
Wasanii
wanapaswa kufa na njaa pale tu kama kazi zao hazikubaliki na hadhira na
hivyo hazinunuliki. Lakini suala la kufichwa na kufunikwa kwa jitahada
za nguvu ya uwezo wa kifedha, mali na mtandao mpana ni la kupingwa kwa
nguvu zote na hadhira. Lazima hadhira iwe ndiyo hakimu pekee wa kazi,
maslahi na mafanikio ya wasanii. Haiwezekani hadhira ionekane ni ya
muhimu tu katika kauli mbiu za kuteka masoko kibiashara lakini
linapokuja suala la mahitaji, hadhira ichaguliwe na fanani nini
inastahili kusikia, kuona, au kula. Hili kamwe haliwezi kuwa chaguo
langu wala la hadhira au Watu.
Ni
chaguo la fanani na la stahili kusikilizwa, kuonwa au kuliwa na huyo
huyo fanani na mafanani wenzake.
Dhihaka inakuwa kubwa zaidi pale jambazi linapoongoza jitihada ya
kutokomeza kazi za vibaka! Kweli mwenye nacho hujitwalia zaidi na sheria
ni kipofu kwa mwenye nacho. Pamoja na yote haya, umma unayo silaha
nzito na mahsusi yenye uwezo wa kuwaangamiza majambazi na kuwatokomeza
vibaka. Silaha yetu ni umoja katika kupinga ufedhuri wa mafanani uchwara
na dhihaka ya majambazi. Anayejitenga na umoja huu, anajindalia upweke
msibani zamu yake ikifika.
Ni
masikitiko kwamba wanaodhurumiwa na kuibiwa wameanguka katika tego la
kale la majambazi na wadhurumaji. Wametegwa wajitenge na umoja na wao
kwa kujua ama kwa kutokujua wakategeka! Wamekubali kuutumikia mkate wa
siku wa kafiri wasijue kwamba kesho safari ya dhuluma yaendelea! Na hawa
watadumu katika safari ya kudhulumiwa milele na hawachomoki ng’o!
Tunaochukizwa na yote yaliyosimuliwa hapo juu, tuungane na waliokwisha
jitambua katika kujinasua na ufedhuri wa madalali uchwara wa sanaa.
Tuwasaidie
kupaza sauti za umoja katika kuwashambulia majambazi. Tuwaonyeshe
mafanani uchwara na majambazi kwamba nguvu haziko kwao bali kwetu
(hadhira). Tulidhirishe kwamba sisi ndiyo tunapaswa kuchagua
tukipendacho maana twalipia muda, huduma na bidhaa.
Tukatae
kuchagulia nini kisikilizwe na masikio yetu, macho yetu yaone nini au
vinywa vile nini na kisha watupigie kauli mbiu za “Chaguo la Watu”
Ijumaa ya Tarehe 31 mwezi huu, tuliowengi hatuendi na kipaumbele cha
kucheza disco, kuangalia wacheza disco au kusikiliza music live bali
tunakwenda kusema hapana: “Unyonyaji haukubaliki na Kufanyiwa machaguo
hakukubaliki”. Tutafanya hivyo kwa sauti kubwa na ya umoja. Tunakwenda
kuthibitisha kuwa ni Sisi ndiyo hadhira na siyo wao.
From:Issa Michuzi
From:Issa Michuzi
No comments:
Post a Comment