Video: Shasha akiongea na GPL kuhusu kuzaa na Diamond.
MREMBO Sasha Juma, 20, kwa sasa anapitia
kipindi cha majuto, analipia gharama ya kujivalisha ubandidu na
kujisingizia kupewa mimba na supastaa, Nasibu Abdul Juma ‘Diamond’.
Sasha, akiwa na macho makavu, alitamka
mbele ya waandishi wetu kuwa mimba hiyo aliyopewa na Diamond,
ilimgharimu kufukuzwa shule akiwa kidato cha nne mwaka jana.
Unadhani Sasha analo tena? Ameshaumbuka
na baada ya simulizi yake ya kutunga kushtukiwa, hivi sasa mrembo huyo
anatishia kujiua.
Mr. Juma ambaye ni baba mzazi wa Sasha,
aliliambia “Huyu mtoto ametishia kujiua, anajua makosa aliyoyafanya.
Anataka kutuvuruga vichwa, ukweli ni kwamba kila alichokisema kuhusu
Diamond ni uongo mtupu.
“Nahisi kuna mtu yupo nyuma yake, sasa
anataka kumtumia ili kumchafua Diamond, upande mwingine akili yangu
inaniambia yule mtoto anataka umaarufu, maana najua yule ni mwigizaji,
sasa pengine anataka kutoka.”
UONGO WA SASHA
Tulipata taarifa kuhusu malalamiko ya
Sasha ambaye alikuwa akidai kupotezewa dira ya maisha na Diamond kwa
sababu alimpa mimba na kumtelekeza na mtoto mwenye umri wa miezi minne.
Baada ya kupata ‘tipu’ hiyo, mwandishi
wetu alimsaka kwa udi na uvumba mpaka Septemba 4, mwaka huu (Jumatano
ya wiki iliyopita) ambapo mrembo huyo alitia maguu kwenye mjengoni.
Baada ya kuwasili makao makuu , Bamaga,
Mwenge, Dar es Salaam, Sasha aliingizwa kwenye chumba maalum chenye
mitambo ya kurekodi sauti na picha kisha akaanza kumwaga simulizi yake.
Alidai kuwa alikutana na Diamond,
Mlimani City, mwaka jana, wakapeana namba za simu kabla ya kuanzisha
uhusiano wa kimapenzi ambao uliwafikisha kwenye ‘kategori’ ya kuparamia
kitandani na kutenda mchezo wa baba na mama pasipo kutumia na kinga.
“Nilipopata mimba Diamond alinishawishi
nisitoe, akaniahidi atanisomesha hata kama nitafukuzwa shule. Baadaye
nilifukuzwa shule, akazidi kunipa moyo kwamba atanilinda. Mimba
ilipokuwa kubwa akapotea, nilipozaa hakujitokeza.
“Diamond akawa siyo yule ambaye alikuwa
ananipa moyo. Alibadilika, hali hiyo ikanifanya nione mwanangu hana
baba, hata cheti za kuzaliwa, sijamwandika Diamond, mtoto wangu nimempa
ubini wa baba yangu, yaani ya Juma.”
NI UONGO MTAKATIFU
Ili kukamilisha habari hiyo ambayo
ilitoka kwenye gazeti hili, toleo la Jumamosi iliyopita, mwandishi wetu
aliwasiliana na baba mzazi wa Sasha (Mr. Juma) ambaye alipoambiwa
kuhusu mwanaye kuzaa na Diamond, alishtuka kisha akasema:
“Unajua yule mtoto sikai naye, anaishi
na mama yake. Mimi sijui chochote ila nashangaa, inawezekanaje apate
mimba mpaka azae mimi baba yake sijui? Ngoja niongee na mama yake.”
Mr. Juma alipiga simu kuzungumza na mama yake Sasha mbele ya mwandishi wetu. Mazungumzo yalikuwa kama ifuatavyo;
MR. JUMA: Habari yako.
MAMA SASHA: Salama tu, za kwako?
MR. JUMA: Namshukuru Mungu, ebwana mbona Sasha kaongea na mwandishi wa habari anasema kapewa mimba na Diamond na amezaa?
MAMA SASHA: Wewe si unajua haya mambo ya vijana?
MR. JUMA: Mambo ya vijana kivipi? Ina maana mtoto anapata ujauzito mpaka anazaa wewe na baba yake hamjui?
MR. JUMA: Mimi baba yake sijui, ndiyo maana nakuuliza wewe, maana nimesikia umekuwa unawasiliana na Diamond kuhusu hili.
MAMA SASHA: Nani kakwambia? Nimeshasema
hayo ni mambo ya watoto, naomba umuulize mwanao vizuri, kama hauna
namba yake nikutumie.
Katika mazungumzo hayo, Mama Sasha,
hakumpa majibu ya moja kwa moja mzazi mwenzake, kuhusu binti huyo
kupata mimba, kuzaa na Diamond kuwa mhusika.
RIPOTI YA WIKI HII
Mr. Juma alifika ofisi za Global
Publishers na kueleza: “Jana (Jumapili iliyopita), nilimchukua Sasha na
kuzungumza naye kwa kirefu, kwa kifupi alikiri kuwa hajawahi kupata
mimba na yule mtoto si wa kwake.
“Mtoto imebainika ni wa dada yake, yaani
mtoto mkubwa wa Mama Sasha ambaye anaitwa Khadija. Kuna kitu cha
kujifunza hapa kuwa Sasha aliwadanganya mpaka watu ambao niliwakabidhi
ili wamsaidie kisanii.
“Kabla sijaongea kwa kirefu na Sasha,
nilizungumza na Thabit Abdul (mwanamuziki wa Five Stars) ambaye
nilimkabidhi kwake kumsimamia kisanii, nikamuuliza inakuwaje mtoto
anapata mimba? Akanijibu hata yeye anashangaa. Kwani hata yeye
alishangaa kumuona Sasha akiwa na picha nyingi amebeba mtoto kwenye
simu yake.
“Akamuuliza umezaa akajibu ndiyo. Hisia
zangu zinazunguka katika mambo mawili, ama aliamua kutunga ili kupata
umaarufu kupitia jina la Diamond au alitumwa na mtu. Jana wakati
nazungumza na Sasha, nilikasirika sana, nikaona hatutafika pazuri.
“Ikabidi nimpigie simu rafiki yangu
mmoja ili amwite azungumze naye. Kweli alimwita wakazungumza, baadaye
yule rafiki yangu akaniambia Sasha kasema anaona mambo yanazidi kuwa
makubwa, kwa hiyo anataka kunywa sumu afe. Namshangaa sana huyu mtoto,
sijui ana kichaa gani?”
UKWELI NI HUU
Kwa mujibu uchunguzi wetu usio na
shaka, mtoto aliyepigwa picha akiwa amebebwa na Sasha, mama yake halisi
ni dada wa mrembo huyo ambaye ni Khadija.
Sasha na Khadija wanaunganishwa na mama yao lakini kila mmoja ana baba yake.
Uchunguzi zaidi ulibaini kuwa kwa sasa
Khadija anaishi na mwanaye mkoani Tanga, huku Sasha akiendelea
kupuyanga ndani ya Jiji la Dar, akiwa hajui tamu wala chungu ya
kunyonyesha, vilevile hajawahi kusikia uchungu wa uzazi wala hatambui
sura ya ‘leba’ ilivyo.
Khadija akizungumza kupitia simu ya Mr.
Juma, huku mwandishi wetu akifuatilia mazungumzo, alisema: “Nikija Dar
nitafika Global, mimi ndiyo mama wa yule mtoto na zile picha Sasha
alipiga na mtoto siku ya arobaini yake.
“Sasha anataka kunisababishia matatizo
na baba mzazi wa mtoto. Mimi kama mama mzazi wa mtoto, simjui Diamond,
kwa hiyo hahusiki chochote na mtoto wangu.”
Aidha, Mr. Juma alisema kuwa alimpigia simu Diamond na kumuweka sawa kuhusiana na tuhuma ambazo binti yake alimsakizia.
“Diamond anajua kila kitu, nimeshaongea
naye na nimejaribu kumtaka atulize munkari, maana ni wazi zile taarifa
zimemchukiza sana. Kweli zimemchukiza.”
DIAMOND ANASEMAJE?
Gazeti hili lilipozungumza na Diamond,
alisema: “Nilishasema simjui huyo Sasha, ahadi yangu ipo palepale,
nitampeleka mahakamani. Amenichafua sana.
“Masharti yangu ni haya, kama anataka nimsamehe aende kweye redio na televisheni akatangaze kwamba sijampa mimba.”
ONYO
Aibu ambayo Sasha anakutana nayo sasa na
tishio la kuburuzwa mahakamani ambalo analikabili kutoka kwa Diamond
ni onyo kwa watu wengine ambao wamekuwa na tabia za kuwasingizia wenzao
ili kujipatia umaarufu.