Blogger Widgets

November 2, 2013

Taarifa Mpya Kuhusu Agness Masogange Kujificha


 Agness Gerald ‘Masogange’.
MAKAMANDA wa vitengo vya kudhibiti madawa ya kulevya kwa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wamemaliza kikao chao jana kujadili mustakabali wa uhalifu ikiwemo hukumu iliyotolewa kwa Mtanzania Agness Gerald ‘Masogange’ aliyekamatwa na malighafi haramu aina ya Ephedrine, Julai 5, 2013 nchini Afrika Kusini kwamba ni ndogo.
 
Taarifa za ndani kutoka Jeshi la Polisi Tanzania zimeeleza kuwa makamanda wa nchi hizo 15 walikutana jijini Arusha kuanzia Jumatatu iliyopita lengo kubwa likiwa kutokubaliana na adhabu zinazotolewa na baadhi ya nchi wanachama kwa wanaokutwa na hatia ya kukamatwa na madawa ya kulevya ‘unga’.

WALICHOJADILI

Kwa mujibu wa chanzo kilicho ndani ambacho kiliomba hifadhi ya jina kwa kuwa si msemaji, makamanda wa nchi hizo walikuwa na kibarua kizito cha kujadili mbinu mbalimbali za kukabiliana na uhalifu pamoja na hukumu inayotolewa kwa watu wanaokutwa na hatia ya kukamatwa na unga.
“Walijadili matukio mengi ya uhalifu likiwemo suala la madawa ya kulevya, wakajadili mbinu za kukomesha biashara hiyo haramu ili waweze kupata suluhisho la kudumu,” kilisema chanzo hicho.
                                                                           
WATAKA HUKUMU KWA NCHI WANACHAMA IWE MOJA

Ilidaiwa kuwa, malighafi aliyokamatwa nayo Masogange na mwenzake kwa nchi nyingine kifungo chake kinafanana na kile cha mtu aliyekamawa na madawa ya kulevya, lakini kwa Afrika Kusini ni cha chini sana.
Chanzo hicho kilizidi kumwaga data kuwa, miongoni mwa masuala yaliyokuwepo kwenye ajenda ni pamoja na umoja katika suala zima la hukumu hususan kwa watuhumiwa wa madawa ya kulevya kwani kumekuwa hakuna uwiano baina ya nchi moja na nyingine ndani ya Jumuiya hiyo.
“Tumeona ilivyokuwa kwa Masogange, nchi nyingi zimepinga kabisa ile hukumu kwani ilikuwa haifanani na kosa husika. Mtu anatozwa faini ya shilingi milioni nne na laki nane (Sh. milioni 4.8) kitu ambacho hakiingii akilini kabisa, makamanda wengi wameonesha kupinga hukumu ile,” kilisema chanzo hicho.

MASOGANGE AJIFICHA

Wakati makamanda wa nchi hizo wakimaliza kikao chao, habari zenye utata zimesambaa kwamba, Masogange alitua Bongo katikati ya mwezi uliopita lakini anaishi Dar au Mbeya kwao kwa kujificha.

Baadhi ya watu, wakiwemo marafiki zake wamekuwa wakisema kwa mkato staa huyo yupo Dar huku wengine wakisema baada ya kutua Dar alikwenda kwao Mbeya kwa sababu hataki kujulikana kuwa amesharudi Bongo.
Mwenyewe anapopatikana kwenye simu na kuulizwa amekuwa akijibu bado yupo Afrika Kusini lakini siku yoyote atatua Dar.

NZOWA ATOA UFAFANUZI

Kamanda wa Kikosi cha Kuzuia na Kupambana na Madawa ya Kulevya Tanzania, Godfrey Nzowa alipoulizwa kwa njia ya simu juzi kuhusu mkutano huo alijibu kuwa yupo safarini kikazi akiwa katika mazingira mazuri atatoa ufafanuzi.
“Nipo safarini kikazi, naomba unitafute siku nyingine nitakupa ufafanuzi mzuri sana,” alisema Kamanda Nzowa ambaye naye ilidaiwa alikuwepo kwenye kikao hicho.

KUMBUKUMBU

Masogange na Mellisa Edward walikamatwa Julai 5, mwaka huu kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Oliver Tambo uliopo Kempton Park jijini Johannesburg  nchini humo wakidaiwa kuingiza madawa ya kulevya aina ya Crystal Methamphetamine yenye thamani ya shilingi bilioni 6.8.
Hata hivyo, mahakama kuu nchini humo ilidai madawa hayo si ya kulevya bali ni malighafi haramu iitwayo Ephedrine ambapo kwa sheria za Afrika Kusini mtu akipatikana na hatia ya kuyaingiza nchini humo ni kifungo cha miezi 32 jela au faini ya shilingi milioni 4.8 kama alivyohukumiwa Masogange ambayo ni ndogo.
Pata habari kama hii kwa ufupi kwenye simu yako ya mkononi ya Vodacom kwa kutuma neno GLOBAL kwenda 15778.
From:Gpl

No comments:

Post a Comment