Stori: Mwaija Salum
STADI wa sanaa za maonesho nchini, Amri Athuman ‘King Majuto’ amesema
ameamua kumtafuta Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya
Kikwete kwa sababu ana siri nzito anayotaka kumpa.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Kikwete.
Akizungumza na Risasi Mchanganyiko juzi jijini Dar es Saalam, mkongwe
huyo alisema ni kweli anahitaji msaada wa trekta ambao anaweza kupewa
na wasaidizi wake, lakini ana mengi anayotaka kumwambia rais.
“Nina mashamba makubwa yenye hekari 11 huko Muheza (Tanga), natarajia
kulima mazao ya biashara lakini sina uwezo wa kununua trekta ndiyo
maana nataka rais anisaidie. Lengo langu ni kuonesha mfano kwa wasanii
wengine. Sanaa ina mwisho wake, siwezi kuigiza milele ndiyo maana
nahitaji sasa kuwekeza kwenye kilimo.
“Pamoja na hilo nina mengi ya siri ninayotaka kuzungumza na rais
kuhusu sanaa yetu. Nitamtafuta kwa juhudi zote na nina imani
nitafanikiwa kuonana naye maana najua rais wetu ni mtu wa watu,” alisema
King Majuto.
King Majuto ni msanii wa vichekesho aliyejizolea umaarufu mkubwa
Bongo, amewahi kutwaa tuzo mbalimbali ikiwemo ya Mkali wa Kuchekesha
iliyotolewa na gazeti hili mwaka juzi.
